Rais ateua Ma DC, awahamisha wengine

0

Rais Samia Suluhu Hassan ameteua na kufanya mabadiliko ya uteuzi kwa wakuu wa wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri, Makatibu Tawala na Kaimu Kamishna Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA).

Kwa Wakuu wa wilaya amemhamisha kituo cha kazi Sixtus Mapunda kutoka wilaya ya Sumbawanga mkoani Rukwa kuwa mkuu wa wilaya ya Temeke mkoani Dar es Salaam.

Mapunda anachukua nafasi ya Mobhare Matinyi ambaye ameteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari – Maelezo na Msemaji Mkuu wa Serikali.

Amemhamisha kituo cha kazi mkuu wa wilaya ya Urambo mkoani Tabora Kenan Kihongosi kwenda kuwa mkuu wa wilaya ya Momba mkoani Songwe.

Kihongosi anachukua nafasi ya Fakii Raphael Lulandala ambaye ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM).

Elibariki Bajuta, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Mamlaka ya Hifadhi ya eneo la Ngorongoro ameteuliwa kuwa mkuu wa wilaya ya Urambo mkoani Tabora kuchukua nafasi ya Kenan Kihongosi aliyehamishiwa Momba.

Rais Samia pia amemteua William Mwakilema, Kamishna wa Uhifadhi wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kuwa mkuu wa wilaya ya Korogwe Mkoani Tanga kuchukua nafasi ya Jokate Mwegelo ambaye ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT).

Nyakia Ally Chirukile ameteuliwa kuwa mkuu wa wilaya ya Sumbawanga ambapo anachukua nafasi ya Sixtus Mapunda aliyehamishiwa Temeke.

Kabla ya uteuzi huo Nyakia alikuwa Katibu Tawala wa Ngorongoro.

Bashungwa ambana Mkandarasi, atoa siku 14

0

Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa ametoa siku 14 kwa Wakala wa Barabara (TANROADS), Bodi ya Usajili wa Makandarasi (CRB) na Bodi ya Usajili ya Wahandisi (ERB) kuhakikisha mkandarasi aliyepewa kazi ya kujenga barabara ya Ibanda – Kajunjumele – Kiwira/Itungi Port (km 32) analeta vifaa na watalaam wote wanaohitajika eneo la mradi kwa mujibu wa mkataba.

Mradi wa barabara hiyo unafadhiliwa na Serikali kwa asilimia 100 kwa gharama ya zaidi ya shilingi Bilioni 38 ambapo unatekelezwa na mkandarasi kutoka kampuni ya M/s AVM-Dillingham Construction International na kusimamiwa na Kitengo cha TECU kutoka Wakala wa Barabara(TANROADS).

Bashungwa ametoa agizo hilo wilayani Kyela mkoani Mbeya mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara hiyo ambayo ipo nyuma ya muda wa mkataba kwa asilimia 25 na kubaini mradi huo una upungufu wa watalaam na vifaa muhimu vinavyohitajika eneo la mradi.

“Naiagiza TANROADS, CRB na ERB kunipa taarifa ndani ya siku hizo na kama mkandarasi akishindwa kutekeleza kama mkataba unavyosema na tutalazimika kuchukua hatua ngumu basi tuzichukue haraka iwezekanavyo”, amesema Bashungwa.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera, amesema kuwa mradi huo ni moja ya mikakati ya Serikali ya kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii mkoani humo kwa kuboresha mtandao wa barabara ili kuongeza ufanisi katika sekta ya usafiri na usafirishaji.

Kwa upande wake, Mhandisi Mshauri kutoka Kitengo cha TECU, Mhandisi Joel Mwambungu, ameeleza kuwa mkataba wa ujenzi na mkandarasi huyo ulisainiwa tarehe 27 Disemba 2022 na alitakiwa kuanza kazi tarehe 30 Machi 2023 mradi unatarajiwa kukamilika ifikapo tarehe 30 Machi 2025.

Ameongeza kuwa hadi sasa mkandarasi  amefanya maandalizi kwa asilimia 15 tu ukilinganisha na mahitaji ya mkataba na kazi zinazoendelea ni kusafisha eneo la ujenzi ambapo ameshamaliza kilometa 5.

Waziri Ummy : Wananchi fanyeni uchunguzi wa awali kwa kupima saratani ya matiti

0

Waziri wa Afya Ummy Mwalimu amewataka wananchi kufanya uchunguzi wa awali wa kupima Saratani ya Matiti ili kujua hali zao na kupata matibabu mapema kwa wenye changamoto hiyo.

Waziri Ummy ameyasema hayo wakati akimwakilisha Makamu wa Rais Dkt. Philip Mpango kwenye Maadhimisho ya Mwezi wa Saratani ya Matiti yaliyofanyika katika viwanja vya Taasisi ya Saratani Ocean Road Jijini Dar es Salaam.

“Wataalamu wanatueleza kwamba mtu anaweza kujichunguza mwenyewe na akiona mabadiliko ya uvimbe katika titi, basi anashauriwa kuwahi katika kituo cha kutolea huduma za Afya kwa uchunguzi zaidi”. – Amesema Waziri Ummy.

Aidha, Waziri Ummy amesema Tanzania inakadiriwa kuwa na wagonjwa wapya wa Saratani takribani Elfu Arobaini na Mbili (42,000) kila Mwaka huku asilimia 38 kati ya hao ndio wanafika katika vituo vya kutolea huduma za Afya.

“Wakati Tanzania tunakadiriwa kuwa na wagoniwa wapya wa Saratani takribani Elfu Arobaini na Mbili (42,000) kila Mwaka, wagonjwa asilimia 38 tu ndio wanafika Hospitali, maana yake katika kila wagonjwa 100 wa Saratani, wagonjwa 38 tu ndio wanafika katika vituo vya kutolea huduma za Afya”. Amesema Waziri Ummy

Pia, Waziri Ummy amesema taarifa ya mwaka 2022/2023, inaonesha kuwa Taasisi ya Saratani Ocean Road ilihudumia wagonjwa wapya takriban 8,779 na asilimia 13 ya wagonjwa hao sawa na wagonjwa 1,141 walikuwa na Saratani ya Matiti.

Jokate ateuliwa Katibu Mkuu UWT

0

Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), imemteua Jokate Mwegelo kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT).

Kabla ya uteuzi huo Jokate alikuwa mkuu wa wilaya ya Korogwe mkoani Tanga.

Pia imemteua Fakii Raphael Lulandala kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) ambapo kabla ya uteuzi huo alikuwa
mkuu wa wilaya ya Momba mkoani Songwe.

Katika hatua nyingine Kamati Kuu imemteua Hamad Khamis Hamad kuwa mgombea wa CCM wa nafasi ya Uwakilishi katika jimbo la Matembwe.

Tunaomba barabara na umeme maeneo ya migodi

0

Mbunge wa Busanda mkoani Geita Mhandisi Tumaini Magesa, ameiomba Serikali kujenga miundombinu ya barabara na umeme kwenye maeneo yenye shughuli za uchimbaji wa madini mkoani humo ili kurahisisha shughuli za uchimbaji madini na kuokoa gharama mbadala.

Magesa ameyasema hayo wakati wa ufungaji wa maonesho ya Sita ya Kimataifa ya Teknolojia ya Madini mkoani Geita na kuyataja maeneo yenye changamoto ya barabara na umeme ambayo ni barabara ya kutoka Buliyankuru – Kahama na Katoro – Magenge – Ushirimbo.

Ameongeza kuwa, kuwepo kwa changamoto hiyo ya barabara na umeme kunapelekea kutumia gharama nyingi katika kuendesha migodi hiyo na kusababisha wachimbaji wadogo kutokuwa na mazingira mazuri kushiriki kwenye shughuli za uchimbaji

Msukuma : Geita hatuna matatizo na Rais Samia

0

Mbunge wa Geita Vijijini Joseph Kasheku (Msukuma) amesema Geita hawana matatizo yoyote na Rais Samia Suluhu Hassan kwasababu yote waliyoyaomba yamefanyiwa kazi na yanaendelea kufanyiwa kazi jimboni kwake.

Msukuma ameyasema hayo wakati wa ufungaji wa maonesho ya Sita ya Kimataifa ya Teknolojia ya Madini mkoani Geita.

Amesema katika jimbo lake la Geita Vijijini, barabara zimejengwa mpaka mtaani, umeme upo na pia kuna taa zimefungwa katika barabara za jimbo hilo.

Aidha, Msukuma ameomba maonesho hayo ya madini yaendelee kufanyika Geita na kutopelekwa sehemu nyingine kama ilivyo kwa maonesho mengine kama Sabasaba na Nanenane ambayo huzunguka mikoa mbalimbali. Msukuma amesema asili ya Dhahabu ni Geita na mkoa huo unaongoza kwa uchimbaji wa madini hivyo haina haja kuyapeleka maonesho hayo sehemu nyingine

Tatizo sio wawekezaji, ni watendaji wa serikali

0

Mbunge wa Msalala Iddi Kassim Iddi, amesema changamoto ya kutofanyiwa kazi kwa miradi mbalimbali ya wawekezaji Serikalini kwa asilimia kubwa inasababishwa na baadhi ya watendaji serikalini na matatizo wanayo wao na sio wawekezaji.

Iddi ambaye pia amemwakilisha Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge, Nishati na Madini, ameyasema hayo wakati wa ufungaji wa maonesho ya Sita ya Kimataifa ya Teknolojia ya Madini mkoani Geita.

Ameongeza kuwa, hata baadhi ya changamoto ya barabara mkoani Geita tayari wawekezaji wameshatoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hizo lakini baadhi wa watendaji serikalini ndio wanaokwamisha ujenzi huo.

Ameiomba Serikali kutunga sera ya msamaha wa kodi kwa wachimbaji wadogo na pia kuondoa ukomo kwa makampuni yanayofanya utafiti wa madini ili kuyapa muda wa kufanya utafiti huo zaidi.