Mkakati wa nne wa Taifa wa Kudhibiti Ukimwi wazinduliwa

0

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amezindua Mkakati wa Nne wa Taifa wa Kudhibiti Ukimwi wa mwaka 2018/2019 hadi mwaka 2022/2023, unaotarajiwa kupunguza maambukizi mapya ya Virusi vinavyosababisha Ukimwi kwa asilimia 75 ifikapo mwaka 2020 na asilimia 85 ifikapo mwaka 2023.

Matokeo mengine yanayotarajiwa kufikiwa kutokana na mkakati huo ni kupungua kwa maambukizi mapya ya Virusi vinavyosababisha Ukimwi miongoni mwa watoto kwa chini ya asilimia tano ifikapo mwaka 2023 na chini ya asilimia 2 ifikapo mwaka 2030.

Waziri Mkuu Majaliwa amezindua mkakati huo kwenye kilele cha maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika Kitaifa jijini Dodoma na kuongeza kuwa matayarisho ya mkakati huo yamezingatia matokeo ya mapitio ya Mkakati wa Tatu wa Taifa wa Kudhibiti Ukimwi wa mwaka 2013/2014 hadi 2017/2018.

Amesema kuwa mbali na matokeo hayo, mkakati huo pia utawezesha kupungua kwa vifo vinavyohusiana na ukimwi kwa asilimia 50 ifikapo mwaka 2020 na asilimia 70 ifikapo mwaka 2023 na kupunguza unyanyapaa ifikapo mwaka 2023 na kuelekea kutokomeza kabisa ifikapo mwaka 2030.

Hata hivyo Waziri Mkuu Majaliwa amesema kuwa mkakati huo wa Nne wa Taifa wa Kudhibiti Ukimwi umewianisha na kupanga programu mbalimbali zinazosaidia mwitikio wa Taifa, zikiwemo afua zinazotekelezwa kupitia mpango wa dharura wa Rais wa Marekani wa Ukimwi (PEPFAR).

Waziri Mkuu Majaliwa ametumia maadhimisho hayo ya siku ya Ukimwi Duniani yanayofanyika kila Disemba Mosi, kuzungumzia faida za kampeni ya Furaha Yangu aliyoizindua mwezi Juni mwaka huu ambapo aliagiza mikoa yote kufanya uzinduzi wa kampeni hiyo kwenye ngazi za mikoa na wilaya.

Amesema kuwa takwimu zinaonyesha kuwa wakati wa uzinduzi wa kampeni hiyo katika mikoa yote nchini, jumla ya wananchi 262,114 walijitokeza kupima ili kujua kama wameambukizwa Virusi vinavyosababisha Ukimwi au la.

Amewahakikishia Watanzania wote kuwa serikali itaendelea kutekeleza na kuboresha huduma za upimaji wa Virusi vinavyosababisha Ukimwi, kuzuia maambukizi ya kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto, matibabu ya magonjwa nyemelezi na kupiga vita unyanyapaa wa aina zote kwa watu wanaoishi na Virusi vinavyosababisha Ukimwi.

Kituo cha huduma kwa pamoja huko Namanga chazinduliwa

0

Rais  John Magufuli na Rais  Uhuru Kenyatta wa Kenya wamezindua kituo cha huduma kwa pamoja mpakani katika eneo la Namanga mpakani mwa Tanzania na Kenya.

Pamoja na kuzindua ofisi za kituo hicho katika pande zote mbili,  Marais hao wamepanda miti ya kumbukumbu na kukagua utoaji wa huduma zikiwemo za forodha na uhamiaji.

Kituo hicho ni miongoni mwa vituo 15  vinavyojengwa katika mipaka ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, kwa lengo la kurahisisha ufanyaji wa biashara miongoni mwa nchi hizo, kuharakisha huduma za mpakani, kuongeza mapato na kuimarisha usalama.

Ujenzi wa kituo hicho cha huduma kwa pamoja mpakani katika eneo la Namanga umefadhiliwa na Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB), Shirika la Maendeleo la Japan (JICA) na Serikali za Tanzania na Kenya ambapo miundombinu ya upande wa Tanzania imegharimu shilingi Bilioni 22.365.

Tangu kianze kutoa huduma,  kituo hicho kimesaidia kupunguza muda unaotumiwa kukamilisha huduma za mpakani  kutoka saa moja hadi dakika 15, na pia kwa upande wa Tanzania ukusanyaji wa mapato umeongezeka kutoka shilingi Bilioni 41 hadi kufikia shilingi Bilioni 58 zinazotarajiwa mwaka huu.

Wakizungumza baada ya kuzindua kituo hicho Rais Magufuli na Rais Kenyatta wamewashukuru wafadhili wa ujenzi huo na wametoa wito kwa Watanzania na Wakenya kuongeza biashara kupitia mpaka huo, huku wakitaka wafanyabiashara wadogo wasibughudhiwe.

“Kenya ni ya tatu kati ya nchi 10 zinazoongoza kwa uwekezaji Tanzania, kwa hiyo Wafanyabiashara wa Kenya wanapopita hapa msiwaone kuwa ni maadui, halikadhalika Tanzania ni yenye mifugo mingi hasa ng’ombe kwa hiyo Watanzania wanapopeleka nyama Kenya nao wasikwamishwe” amesisitiza Rais Magufuli.

“Sisi tujione wana Afrika Mashariki, tuzilete nchi zetu pamoja na tuutumie umoja wetu wa watu takribani Milioni 200 kufanya biashara na kunufaika, sisi viongozi wajibu wetu ni kurahisisha biashara sio kukwamisha, na nyie wananchi muwe huru kufanya biashara zenu ilimradi msivunje sheria na kufanya biashara haramu” amesema Rais Kenyatta.

Aidha, Rais Magufuli ameahidi kushughulikia tatizo la maji katika eneo la Namanga kwa kupeleka maji  kutoka Longido ambako serikali imejenga mradi mkubwa wa maji uliogharimu shilingi Bilioni 15.

Rais Magufuli pia ameishukuru AfDB baada ya Mkurugenzi Mkuu wa benki hiyo katika ukanda wa Afrika Mashariki, – Gabriel Negatu kueleza kuwa benki hiyo imeridhia kutoa fedha kwa ajili ya kutekeleza mradi wa ujenzi wa barabara ya Malindi – Lungalunga – Tanga – Pangani – Bagamoyo inayounganisha nchi za  Tanzania na Kenya, na mradi wa barabara ya Rumonge – Manyovu – Kasulu – Kibondo – Nyakanazi inayounganisha nchi za Tanzania na Burundi.

Marais Magufuli, Museveni na Kenyatta wakutana

0

Rais John Magufuli amekutana na Rais Yoweri Museveni na Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya ambao walikua jijini Arusha kwa ajili ya kuhudhuria mkutano wa 20 wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ambao hata hivyo umeahirishwa hadi Disemba 27 mwaka huu.

Mara baada ya kikao cha ndani kilichofanyika katika moja ya kumbi za watu mashuhuri ndani ya Kituo cha mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC), Marais wote watatu walisafiri kwa gari moja hadi Ikulu ndogo ya Arusha.

Rais Museveni amesema kuwa mkutano huo umeahirishwa kutokana na mmoja wa wanachama wa jumuiya hiyo ambaye ni nchi ya Burundi kutohudhuria, ilihali mkataba wa jumuiya hiyo unataka maamuzi yafanywe na wanachama wote kwa pamoja.

“Tuliamua kuahirisha mkutano kwa leo kwa sababu mmoja wetu ambaye ni Burundi hakuja, tumeahirisha mkutano mpaka tarehe 27 Disemba mwaka 2018 wakati sisi wote tutakapokuwepo, kwa sababu mkataba wa Afrika Mashariki unasema mambo mawili, moja lazima tuwe na mkutano mmoja wa kawaida kila mwaka na ndio huu wa leo, lakini vile vile uamuzi wowote utakaofanyika lazima wanachama wote wawepo, kwa hiyo kama mmoja hayupo sio vizuri kuendelea, inakuwa inakwenda kinyume na mkataba”, amesema Rais Museveni.

Akiwa mkoani Arusha, Jumamosi Disemba Mosi mwaka huu, Rais Magufuli na Rais Kenyatta watafungua kituo cha huduma za pamoja mpakani katika eneo la Namanga mpakani mwa Tanzania na Kenya.

Wanaowapa ujauzito Wanafunzi Nyang’hwale kusakwa

0

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amemuagiza mkuu wa wilaya ya Nyang’hwale mkoani Geita, -Hamim Gwiyama kufanya operesheni katika kila kijiji wilayani humo ili kuwabaini watu waliowapa wanafunzi ujauzito na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria.

Waziri Mkuu Majaliwa ametoa agizo hilo wakati wa ziara yake wilayani Nyang’hwale baada ya kusomewa taarifa iliyoonyesha kuwa wanafunzi wengi wa kike wamekua wakikatisha masomo yao baada ya kupata ujauzito.

Akizungumza na wakazi wa wilaya hiyo katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Sabasaba, Waziri Mkuu Majaliwa ameelezea kusikitishwa na vitendo vya wanafunzi wa kike kupata ujauzito huku wahusika wakiachwa bila ya kuchukuliwa hatua yoyote.

Amesisitiza kuwa serikali haiwezi kulifumbia macho jambo hilo na kuwataka wakazi wa wilaya ya Nyang’hwale kushirikiana katika kuwalinda watoto wao wa kike ili wasipate ujauzito na kwamba serikali itawachukulia hatua watendaji wote nchini ambao katika maeneo yao watoto wa kike watabainika kuwa na ujauzito.

Wanafunzi 72 wamepata ujauzito katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2016 hadi 2018 wilayani Nyang’hwale mkoani Geita .

Cavaliers yaandamwa na matokeo mabovu

0

Jinamizi la matokeo mabovu limeendelea kuwaandama makamu bingwa wa Ligi Kuu ya kulipwa ya mpira wa kikapu nchini Marekani (NBA) timu ya Cleveland Cavaliers baada ya kutandikwa alama 100 kwa 83 na Oklahoma City Thunder katika mchezo uliochezwa kwenye dimba la Chespeake Energy mjini Oklahoma City.

Nyota wa mchezo huo alikuwa Russel Westbroo aliyeifungia Oklahoma alama 23 na kucheza mipira iliyorudi yani Rebounds 19 huku akitoa pasi za kufunga 15 zilizotosha kulizamisha jahazi la Cavaliers lililokuwa likiongozwa na Jordan Clarkson aliyefunga alama 25.

Huo unakuwa mchezo wa 16 kwa Cavaliers kupoteza katika michezo 20 waliyocheza tangu kuanza kwa msimu huu, wakishika nafasi ya mwisho kwenye msimamo wa Kanda ya Mashariki inayoongozwa na Toronto Raptors.

Cavaliers wameyumba kwa kiasi kikubwa baada ya kuondoka kwa aliyekuwa nyota wao Lebron James aliyetimkia Los Angeles Lakers.

Katika matokeo mengine , wakongwe Chicago Bulls wameshindwa kutamba ugenini baada ya kula mweleka wa alama 116 kwa 113 mbele ya Milwaukee Bucks wakati Washngton Wizards wakipokea kipigo cha alama 125 kwa 104 kutoka kwa New Orlean Pelicans huku Dallas Mavericks wakiinyuka Huston Rockets alama 128 kwa 108 na San Antonio Spurs wamelala kwa alama 128 kwa 89 mbele ya Minasota Timberwolves.

Huko Barclays Center mjini Brooklyn – New York, wenyeji Brooklyn Nets wamekiona cha moto kwa kutandikwa alama 101 kwa 91 na Utah Jazz wakati Philadelphia 76ERS wakiishikisha adabu New York Knicks kwa kuitandika alama 117 kwa 91 na Atlanta Hawks wameshindwa kutamba ugenini na kunyukwa alama 108 kwa 94 na Charlote Hornets.

Malipo ya korosho kuanza kesho baada ya uhakiki

0

Serikali imesema itaanza malipo ya wakulima wa zao la korosho kuanzia kesho Novemba 14 baada ya kukamilika kwa zoezi la uhakiki wa wakulima walio kusanya korosho zao katika vyama vya ushirika vya msingi.

Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga amesema hayo mkoani Mtwara alipokuwa akizungumza na wadau wa zao hilo na kusema serikali inataka kuanza malipo ya wakulima hao kesho endapo watakamilisha zoezi la uhakiki wa wakulima waliokusanya korosho zao katika vyama hivyo.

 Waziri Hasunga, Naibu Waziri wa Kilimo Inocent Bashungwa na uongozi mzima wa wizara hiyo umewasili mkoani Mtwara lengo ikiwa ni kuhakiki kiasi cha korosho kilichokusanywa katika vyama vikuu mkoani humo.

Kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Mtwara Gelasius Byakanwa amewatoa hofu wadau ambao wananufaika na biashara ya zao hilo.

Cheyo, Mbatia, Shibuda na Rostam wakutana na Rais

0

Rais John Magufuli amekutana na kufanya mazungumzo na wanasiasa John Cheyo, James Mbatia, John Shibuda pamoja na mfanyabiashara Rostam Aziz Ikulu jijini Dar es salaam.

Baada ya mazungumzo hayo, Rostam Aziz amempongeza Rais Magufuli kwa uongozi bora kwa kuwa amekuwa akitengeneza misingi imara ya uchumi unaokua kwa uhakika zaidi kwa kujenga miundombinu ya barabara, reli na bandari ambayo ni muhimu kwa ukuaji wa uchumi na kuzalisha ajira.

Ameongeza kuwa anaunga mkono jitihada zinazofanywa na Rais Magufuli katika kuwaletea Watanzania maendeleo, huku akibainisha kuwa jukumu la wafanyabiashara ni kutumia fursa nyingi zilizopo katika viwanda, ujenzi na nyinginezo.

“Tunamuunga mkono Rais kwa kuhakikisha Watanzania tunawekeza katika nchi yetu, kukuza uchumi wetu, hilo ndilo la msingi kwa sisi wafanyabiashara” amesema Rostam Aziz.

Naye mwenyekiti wa Kituo cha Demokrasia nchini (TCD) na Mwenyekiti wa Chama cha NCCR Mageuzi, – James Mbatia amesema kuwa katika kutekeleza malengo 17 ya dunia, Tanzania inafanya vizuri katika lengo la elimu ambalo linazungumzia elimu bora na shirikishi.

Mbatia amesisitiza kuwa Watanzania wote wana kila sababu ya kuendelea kuijenga nchi yao kwa mawazo ya pamoja yanayozingatia ujumbe uliomo katika wimbo wa Taifa unaosisitiza hekima, umoja na amani.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa nchini John Shibuda amesema kuwa amekutana na Rais Magufuli ili kumpongeza kwa uamuzi mzuri alioufanya kutatua tatizo la soko la korosho na kumhakikishia kuwa vyama vya siasa vinamuunga mkono kwa uongozi mzuri unaolenga kurekebisha dosari za mmomonyoko wa maadili ndani ya serikali na taasisi mbalimbali vikiwemo vyama vya siasa.

“Katika miaka mitatu, Rais Magufuli amerejesha sifa ya utaifa wetu ya kuwa nchi ya kuaminika na kusadikika na amekweza ari ya uhuru na kujitegemea, tulikuwa na hali duni na dumavu ya maendeleo na ustawi wa jamii, tulikuwa na hali ambayo maendeleo yetu hayawiani na maliasili tulizonazo na rasilimali tulizonazo” amesisitiza Shibuda.

John Cheyo ni Mwenyekiti wa Chama Cha UDP ambaye amempongeza Rais Magufuli kwa msimamo na ujasiri aliouonesha katika kipindi cha miaka mitatu ya uongozi wake na ametaka Watanzania wajivunie kuwa na Rais ambaye ameonesha dhamira njema ya kufikia nchi ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.

“Sisi Watanzania ni lazima tujivunie Rais tuliyenae, ni Rais anayetoa maamuzi, hata kama yatakuwa magumu kiasi gani, akiamua kusema tunakwenda kujenga Stieglers’ Gorge tutakwenda, akiamua kuwa tunakwenda kujenga standard gauge tunakwenda, akiamua watoto watasoma bure kuanzia darasa la kwanza hadi sekondari inafanyika, na katika miaka mitatu hii imedhihirika kuwa maamuzi yake yanalisaidia Taifa sana” amesema Cheyo.

 

 

 

Tanzania kupokea Watalii 10,000 kutoka Shanghai

0

Bodi ya Utalii Nchini (TTB) imesaini makubaliano na kampuni ya Touchroad International Group ya nchini China kwa ajili ya kusafirisha watalii elfu kumi kutoka jiji la Shanghai kutembelea Tanzania mwaka 2019 kwa kutumia ndege maalum.

Taarifa iliyotolewa na wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imesema kuwa makubaliano hayo yamesainiwa wakati wa mikutano ya kutangaza utalii wa Tanzania katika soko la China.

Mikutano hiyo ni matokeo ya jitihada za balozi wa Tanzania nchini China kwa kushirikiana na TTB ambapo katika mkutano wa kwanza uliofunguliwa na Naibu Katibu Mkuu wa wizara ya Maliasili na Utalii Dkt Aloyce Nzuki, zaidi ya washiriki mia mbili wamejitokeza zikiwemo kampuni za utalii, mawakala wa usafirishaji, mashirika ya ndege na vyombo vya habari.

Wakati wa mkutano huo, Mkurugenzi wa Bodi ya Utalii nchini Devotha Mdachi ametoa mada maalum kuhusu vivutio vya utalii vilivyopo nchini pamoja na fursa za uwekezaji katika sekta ya utalii, huku kampuni za utalii kutoka Tanzania zikipata fursa ya kuelezea gharama zao za utalii kwa soko la China.

Nalo Shirika la Ndege nchini (ATCL) limetumia mkutano huo kutangaza mpango wake wa kuanza safari za moja kwa moja kutoka Tanzania hadi China katika mji wa Guangzhou mwezi Februari mwaka 2019.

Mikutano ya kutangaza utalii wa Tanzania katika soko la China inaendelea katika miji mingine nchini humo ikiwa ni pamoja na Guangzhou, Hong Kong, Chengdu na Beijing.