CRDB kuwafikiria wachimbaji wadogo

0

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, – Abdulmajid Nsekela amesema kuwa  kwa muda mrefu imekua ni vigumu kuwakopesha wachimbaji wa madini nchini kutokana na wachimbaji hao kutokuwa na makazi ya kudumu.

Nsekela ametoa kauli hiyo jijini Dar es salaam, wakati wa mkutano wa wachimbaji wadogo wa madini, wafanyabiashara na wadau wa sekta ya madini, mkutano uliokuwa na lengo ya kujadili changamoto mbalimbali zinazowakabili wachimbaji wadogo wa madini na namna ya kuzitatua changamoto hizo.

Amesema kuwa hatua ya wachimbaji hao wa madini kutokuwa na makazi ya kudumu, inawawia vigumu watendaji wa benki hiyo ya CRDB kuwafuatilia ili kuwapatia mikopo.

Hata hivyo Mkurugenzi Mtendaji huyo wa Benki ya CRDB, – Abdulmajid Nsekela  amesema kuwa pamoja na ugumu huo,  bado ipo nafasi ya kuzungumza na wachimbaji hao wa madini kwa lengo la kuona  namna ya kuweza kuwapatia mikopo kuanzia hivi sasa.

Makundi kombe la Shirikisho yapangwa

0

Timu tatu za mpira wa miguu kutoka nchini Morocco zimepangwa kwenye kundi moja katika hatua ya makundi ya kombe la Shirikisho Barani Afrika katika droo iliyofanyika Januari 21 mwaka huu.

Katika kundi A, bingwa mtetezi wa michuano hiyo Raja Casablanca wamepangwa na timu ya Renaissance Berkane na Hassania Agadir,  wakiwa pamoja na timu ya As Otoho Oyo ya Congo Brazzaville.

Kundi  B zipo timu mbili za Tunisia,  ambazo ni bingwa wa kihistoria wa michuano hiyo CS Sfaxien na bingwa mara mbili wa kombe hilo la Shirikisho Barani Afrika, -Etoile Du Sahel.

Timu nyingine mbili zinazounda kundi hilo ni Salitas ya Burkina Faso  na Enugu Rangers kutoka nchini Nigeria.

Nalo  kundi C, timu ya Nkana FC ya Zambia itacheza na Zesco United pamoja na timu za Al Hilal ya Sudan na miamba ya Asante Kotoko ya nchini Ghana.

Kundi la  D linaundwa na timu za Zamalek ya Misri, Hussein Dey ya Algeria, Petro Atletico ya Angola na Gor Mahia kutoka  nchini Kenya.

Hatua ya makundi ya michuano hiyo itaanza mwezi Februari mwaka huu  ambapo michezo mitatu itapigwa ndani ya kipindi cha mwezi huu huku michezo ya marudiano ikichezwa mwezi Machi.

Wadau watoa ushauri kwenye sekta madini

0

Wadau wa sekta ya madini nchini wameishauri serikali  kuwawezesha wachimbaji wadogo wa madini kwa kuondoa kodi mbalimbali ambazo zimekua zikiwaumiza ikiwa ni pamoja na Kodi ya Ongezeko la thamani (VAT).

Wadau  hao wametoa  ushauri huo jijini Dar es salaam wakati wa mkutano wa wachimbaji wadogo wa madini, wafanyabiashara na wadau wa sekta ya madini, mkutano uliokuwa na lengo ya kujadili changamoto mbalimbali zinazowakabili wachimbaji wadogo wa madini na namna ya kuzitatua.

Wamesema kuwa kuwepo kwa kodi na tozo nyingi zinazotozwa na taasisi mbalimbali kunasababisha vitendo vya utoroshwaji wa madini.

Naye mmoja wa wadau hao Mutalemwa Titus amesema kuwa kwa  kipindi cha miaka mitatu wameshindwa kuuza madini yao kutokana na wizara ya Madini kuwakatalia kuyeyusha madini hayo aina ya Tin, hivyo kumuomba Rais Magufuli kuingilia kati suala hilo.

Muinjilisti Solomoni Mihayo ni Mdau wa madini kutoka mkoani Geita, yeye ametaja njia mbalimbali zinazoweza kutumiwa na watu wasio waaminifu kusafirisha madini nje ya nchi ikiwa ni pamoja na  madini yenye thamani kubwa kufungwa kwenye matairi ya akiba ya magari na  kuwekwa kwenye vioo vya kuongozea  magari.

Watanzania watakiwa kuiunga mkono serikali

0

Mkuu wa mkoa wa Dar es salaam, – Paul Makonda ametoa wito kwa Watanzania wote kuendelea kuunga mkono jitihada zinazofanywa na serikali za kuiletea nchi maendeleo na kuifanya iweze kujitegemea.


Makonda ametoa kauli hiyo jijini Dar es salaam wakati wa mkutano wa wachimbaji wadogo wa madini, wafanyabiashara na wadau wa sekta ya madini.


Mkuu huyo wa mkoa wa Dar es salaam ametumia mkutano huo kuwaomba Watanzania wote kuendelea kuwa wazalendo hasa katika kuitetea nchi yao mahali popote walipo na wale wenye nia ya kuitangaza nchi vibaya kuacha kufanya hivyo.


Amempongeza Rais John Magufuli na serikali yake kwa kazi nzuri ya kuliletea Taifa maendeleo ikiwemo ile ya kuboresha miundombinu ya aina mbalimbali.


Ufunguzi wa mkutano huo wa wachimbaji wadogo wa madini, wafanyabiashara na wadau wa sekta ya madini pia umehudhuriwa na Rais John Magufuli, Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, viongozi mbalimbali wa serikali, siasa pamoja na wale wa kidini.

Zanzibar yapata neema kwenye umeme

0

Baraza la Mawaziri limeridhia utozwaji wa kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kwa kiwango cha asilimia sifuri kwenye umeme unaouzwa na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa Shirika la Umeme la Zanzibar (ZECO) na kufuta malimbikizo ya deni la kodi ya VAT lililofikia shilingi Bilioni 22.9 kwa TANESCO kwenye umeme uliouzwa ZECO.

Baraza la Mawaziri limefanya uamuzi huo Ikulu Jijini Dar es salaam, katika kikao kilichoongozwa na Rais John Magufuli na kuhudhuriwa na Makamu wa Rais  Samia Suluhu Hassan, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Ali Mohamed Shein, Katibu Mkuu Kiongozi Balozi John Kijazi na Mawaziri.

Akizungumza baada ya kikao hicho Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri Rais John Magufuli amesema kuwa baada ya kufanya uamuzi huo Waziri wa Fedha na Mipango Dkt Philip Mpango atawasilisha marekebisho madogo ya sheria ya VAT sura ya 148 kupitia sheria ya fedha ya mwaka 2019 ili umeme unaouzwa Zanzibar utozwe VAT kwa kiwango cha asilimia sifuri.

“Kwa hiyo madeni yatakayokuwa yanadaiwa kwa Zanzibar ni yale madeni ya kulipia umeme, umeme wametumia kiasi fulani wanalipa kama wanavyolipa wa maeneo mengine kwa mfano wanavyolipa Dar es salaam, suala la kutoza VAT sasa halipo na katika hilo kwa sababu kulikuwa na deni ambalo lilikuwa limefika shilingi Bilioni 22.9, sisi Baraza la Mawaziri tutapeleka mapendekezo Bungeni kwamba lisamehewe kwa sababu lipo ndani ya bajeti ya mwaka huu wa 2018/2019, kwa hivyo litapunguza mapato yatakayotakiwa kukusanywa na serikali”,  amesema Rais Magufuli.

Kwa upande wake Dkt Shein amesema kuwa pamoja na kuridhia utozaji wa VAT kwa kiwango cha asilimia sifuri, Baraza la Mawaziri pia limekubaliana kuwa Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan ataitisha vikao vya kuzungumzia masuala ya Muungano kila mara kunapokuwa na hoja ya masuala ya Muungano ili kujadili na kutoa uamuzi.

“Tungependa sana mambo haya yafanyike vizuri kwa sababu pande mbili za Muungano zinatuhusu sote, hili ni muhimu kwa sababu mambo yakikusanyika mengi wananchi wanahisi hatusaidii jitihada zao, kwa hivyo tumeridhia kuwa masuala ya Muungano ambayo yapo chini ya Makamu wa Rais, wakae pamoja wayajadili ili yapate uamuzi wa pande zote mbili” amesema Dkt Shein.

Wakati huo huo, Rais Magufuli amemuapisha Anjella Kairuki kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Uwekezaji.

Kairuki ameapishwa kabla ya kuanza kwa kikao hicho cha Baraza la Mawaziri, kufuatia mabadiliko madogo yaliyofanywa na Rais Magufuli Januari Nane mwaka huu ambapo Kairuki aliyekuwa Waziri wa Madini aliteuliwa kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Uwekezaji.

Pienar kuendesha programu za michezo nchini

0

Mchezaji wa zamani wa klabu ya Everton ya England, – Steven Pienar anatarajiwa kuendesha programu maalumu za michezo kwa timu za vijana za mpira wa miguu nchini.

Mkurugenzi wa Utawala na Udhibiti wa SportPesa Tanzania, –  Tarimba Abbas  amewaambia waandishi wa habari jijini Dar es salaam kuwa Pienar atakuwepo nchini wakati wa michuano ya kombe la SportPesa ambapo ataitumia fursa hiyo kuendesha programu hizo ikiwemo kufanya mazoezi na timu ya Taifa ya vijana wenye umri wa chini ya miaka 17.

Akizungumzia mashindano hayo ya kombe la SportPesa ya mwaka huu, Tarimba amesema kuwa ili kuendana na ushindani unaoonyeshwa na timu kutoka nchini Kenya, wameamua kuendesha mashindano hayo katikati ya msimu wa Ligi Kuu Tanzania Bara ili kuzipa nafasi timu za Tanzania kuonyesha ushindani.

Nao viongozi wa Mashirikisho ya nchi zinazotoa timu shiriki kwenye mashindano hayo wamezitaka timu zao kuonyesha ushindani.

Mashindano hayo ya kombe la SportPesa yanaanza kutimu vumbi Jumanne Januari 21 ambapo timu Nane kutoka Tanzania na Kenya zitachuana.