Finland kutoa Shilingi Bilioni 24 kwa Wakulima wadogo wa miti

0
502

Serikali ya Finland  inatarajia kutoa Euro 9.5 sawa na Shilingi Bilioni 24, kwa ajili ya mradi wa  awamu ya Pili wa Panda Miti Kibiashara utakaodumu kwa  muda wa miaka minne kwa ajili ya Wakulima wadogo wa miti wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini.

Akizindua  awamu ya Pili ya mradi huo huko Mafinga wilayani Mufindi mkoani  Iringa, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Constantine Kanyasu ameiagiza  Idara ya Misitu na Nyuki ambayo ndiyo msimamizi Mkuu wa mradi  huo  kwa niaba ya Wizara, kuusimamia vizuri.

Naibu Waziri Kanyasu amewataka  Wataalamu wote watakaokuwa kwenye utekelezaji wa  mradi huo wa  awamu ya Pili wa Panda Miti Kibiashara, kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia thamani ya fedha iliyotolewa.

Katika awamu ya kwanza ya mradi huo, Finland ilitoa Euro Milioni 19.5 sawa na Shilingi  Bilioni 40 kati ya mwaka 2014 na 2018, ambapo kupitia uwezeshaji  huo  jumla ya hekta Elfu 12 za miti bora zimepandwa na zinamilikiwa na Wananchi zaidi ya Elfu Tisa.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri  huyo wa Maliasili na Utalii ameishukuru Serikali ya Finland kwa kufadhili mradi mwingine wa kuongeza mnyororo wa thamani kwa mazao ya misitu  uitwao FORVAC, mradi unaotekelezwa na wizara hiyo katika wilaya Kumi za mikoa ya  Tanga, Dodoma, Lindi na Ruvuma.