Bunge lamsamehe Masele

0
271

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limepitisha azimio la kumsamehe Makamu wa Kwanza wa Rais wa Bunge  la Afrika  ambaye pia ni Mbunge wa Shinyanga Mjini, – Stephen Masele  aliyekuwa akikabiliwa na tuhuma  mbalimbali.

Bunge limefikia uamuzi huo jijini Dodoma,  baada ya Kamati ya  Haki, Maadili  na Madaraka ya Bunge  kukamilisha kazi ya kumhoji mbunge huyo na kumtia hatiani kwa  makosa manne anayodaiwa kuyatenda akiwa  nchini Afrika Kusini  ya   kudharau kiti cha Spika, kuchonganisha Mihimili ya Dola, uongo na utoro Bungeni,  jambo lililokuwa likiharibu taswira ya nchi.

Awali  akiwasilisha taarifa ya Kamati ya  Haki, Maadili  na Madaraka ya Bunge, Mwenyekiti wa kamati hiyo Emanuel Mwakasaka amesema kuwa Mbunge Masele amepatikana na hatia ya kutenda makosa hayo, na hivyo akaliomba Bunge limpe adhabu ya kusimamishwa  kuhudhuria mikutano mitatu ya bunge ili iwe onyo kwa Wabunge na Viongozi wengine.

Baada ya Mwakasaka kuwasilisha taarifa yake, Spika wa Bunge Job Ndugai akatoa nafasi kwa Mbunge Masele kuzungumza ambaye pamoja na mambo mengine ameliomba radhi Bunge na  Viongozi wote, kutokana na usumbufu uliojitikeza wakati wa mgogoro huo.

Spika Ndugai ameipongeza kamati hiyo  ya Haki, Maadili  na Madaraka ya Bunge kwa kazi kubwa iliyoifanya na kuliomba Bunge kumsamehe mbunge huyo.