Kiongozi wa upinzani katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC), – Moise Katumbi amerejea katika jamhuri hiyo baada ya kuishi uhamishoni kwa muda wa takribani miaka mitatu.
Katumbi ambaye ni Gavana wa zamani wa jimbo lenye utajiri mkubwa wa madini la Katanga, alipanga kurejea DRC mwaka 2018 kwa ajili ya kugombea Urais, lakini alizuiwa kurejea nchini humo katika eneo la mpaka wa Jamhuri hiyo na Zambia na vikosi vilivyokua vikimtii Rais Joseph Kabila.
Maelfu ya Raia wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo wamejitokeza katika barabara mbalimbali zinazotoka na kuingia katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Lubumbashi kwa lengo la kumlaki Katumbi huku wakiimba nyimbo na kucheza.
Katumbi alijiuzulu nafasi ya Ugavana wa jimbo la Katanga mwaka 2015, ili aweze kugombea kiti cha Urais, hata hivyo mwaka 2016 aliikimbia nchi hiyo baada ya kutokea tofauti baina yake na Rais Kabila.
Baada ya kukimbia DRC, mahakama nchini humo ilimuhukumu kifungo cha miezi 36 jela bila yeye kuwepo, baada ya kupatikana na hatia ya kuuza mali mbalimbali katika mji wa Lubumbashi.
