Serikali ya Tanzania kuwalipa wateja wa benki ya FBME

0
373

Naibu  Waziri wa Fedha na Mipango Dkt Ashatu Kijaji  amesema kuwa serikali ya Tanzania  na serikali ya Cyprus  zimekubaliana  kuwalipa  wateja wa Benki ya FBME baada ya serikali ya Tanzania kuamua kuifilisi benki hiyo.

Akijibu swali Bungeni jijini Dodoma, Dkt  Kijaji amesema kuwa kwa mujibu wa sheria ya mabenki na taasisi za fedha ya mwaka 2006, wateja wanaoweka fedha zao ndani ya benki au taasisi za fedha ni lazima walipwe amana zao, pindi benki ama taasisi husika ya fedha itakapofilisiwa.

Dkt  Kijaji amewataka wateja ambao wameweka  amana zao zaidi ya Shilingi Milioni Moja na Nusu katika benki hiyo ya FBME kuwa na subira wakati serikali ikiendelea  na utaratibu wa kisheria wa kuhakikisha  amana hizo zinalipwa .

Pia amewaondoa hofu Watanzania wote kuwa Benki zilizopo nchini na taasisi nyingine za Kifedha ziko salama, hivyo hawana sababu ya kuwa na hofu ya kuweka fedha zao  benki.

Bunge linaendelea na mkutano wake wa 15 jijini Dodoma ambapo Wabunge wanaendelea kujadili  bajeti za wizara mbalimbali kwa mwaka wa fedha wa 2019/2020.